Tumeokolewa kwa imani, lakini imani ni nini?

Tumeokolewa kwa imani, lakini imani ni nini?

Ni vigumu sana kueleza imani ni nini kwa maneno machache tu, lakini kuna mambo machache muhimu ambayo yanaweza kutusaidia kuielewa vizuri.

7/6/20185 dk

Na Ukristo wa Utendaji

Tumeokolewa kwa imani, lakini imani ni nini?

Imani ni nini? Hili linaweza kuonekana kuwa swali gumu, kwani imani si kitu tunachoweza kuona au kugusa, na inaweza kumaanisha mambo tofauti kwa watu tofauti! Lakini imani ina maana gani kwa Mkristo?

Imani ni kuchagua kuamini

Kwanza kabisa, imani ya Kikristo inamaanisha kwamba tunaamini kuwa Biblia ni ya kweli, ni Neno la Mungu kwa wanadamu, na imejaribiwa na haibadiliki. Imani pia ni tumaini kamili kwa Mungu, katika upendo wake kwangu, na katika uwezo wake wa kunisaidia bila kujali kinachonipata maishani. Lakini pasipo na imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu  lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba uwapa thawabu wale wamtafutao.”  Waebrania 11:6

Imani ni uamuzi wa kuamini, ni chaguo, sio hisia. Ninachagua kumwamini Yesu Kristo, kwamba alikufa kwa ajili ya dhambi zangu, na kwamba kwa kumwamini, dhambi zangu zitasamehewa. Ahadi iko wazi. "Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa mwanawe pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele." Yohana 3:16. Ni imani katika Mtu ambayo huwaokoa wale wanaoamini, sio imani katika dini fulani au kanuni.

Kila Mkristo atakubali kwamba wokovu ni zawadi, si kitu ambacho tunaweza kupata kwa jitihada zetu wenyewe.  “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya Imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu. Wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.”  Waefeso 2:8-9.

Ikiwa nimetenda dhambi, hatua ya kwanza, muhimu sana ni kukiri, kujuta kwa yale niliyofanya na kuacha dhambi yangu. Lakini bado siwezi kujiokoa! “Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele.” Warumi 6:23. Ili kupokea zawadi hii, lazima niamini na kukubali kibinafsi zawadi ya Mungu kwangu katika Mwanawe. Msamaha wa dhambi ni mwanzo mzuri na huleta furaha kuu kwa kila muumini wa kweli wa Yesu.

Je, ni nini kinachofuata?

Kwa hiyo ninaokolewa kwa neema ninapochagua kuamini. Nini kitatokea baadaye? Je, bado ninahitaji imani? Ndiyo! Ninahitaji imani kama ninataka kuishi maisha yanayompendeza Mwokozi niliyemwamini. Ingawa dhambi zangu zimesamehewa, bado nitajaribiwa mara nyingi na dhambi katika asili yangu ya kibinadamu.

Mstari unaofuata katika Waefeso 2 unatuambia nini mipango ya Mungu kwa ajili yetu baada ya kutoa maisha yetu kwa Mungu. “Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo.” Waefeso 2:10. Kwa hiyo Mungu amepanga jambo kubwa zaidi, na la ajabu zaidi kwa ajili yetu baada ya kumwamini kwa ajili ya msamaha.

Pia imeandikwa katika Warumi 5:10: “Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya mwana wake; Zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake.” Maisha ya Yesu yalikuwa Maisha ya vitendo. Kuokolewa na Maisha yake, napaswa kuwa na Imani kwamba ataniongoza katiika matendo. Paulo anaita utii wa Imani. (Warumi 1:5)

Yesu ndiye Mfano wetu mkuu, na ndiye aliyeanzisha imani yetu na atakayeimaliza kikamilifu. (Waebrania 12:2.) Mashujaa wote wa imani katika Agano la Kale walitenda kwa imani yao. Walifanya jambo. Kila mmoja wao aliamini - na akatenda! Kwa imani Nuhu alitengeneza safina, kwa imani Ibrahimu alitii, na kadhalika. (Waebrania 11.)

Chukua hatua

Yohana anaandika: “Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu.” Yohana 1:4. Ni nuru hii ya maisha ya Yesu ambayo ninahitaji kutembea ndani yake - kuchukua hatua! Ikiwa kweli nataka kutii sheria nzuri za Mungu za maisha zinazopatikana katika Neno Lake, hivi karibuni nitajikuta katika vita dhidi ya dhambi ambayo ninaipata ndani yangu, katika asili yangu. Hii ndiyo inaitwa vita njema ya imani katika 1Timotheo 6:12.

Ili kushinda vita hivi, ninahitaji kuamini katika nguvu iliyo nje yangu, katika uwezo wa Roho Mtakatifu, na katika Yesu ambaye ameahidi kwamba anaweza kuniokoa kabisa. ( Waebrania 7:25 ) Haihusiani na hisia zangu, ambazo zinaweza kupanda na kushuka. Lakini ninapomwamini Mungu, na kuchukua uamuzi thabiti wa kutii sheria zake zinazopatikana katika Biblia, hata dhidi ya hisia zangu au ufahamu wangu wa kibinadamu, basi Mungu huchukua hatua pia! Yeye hutuma neema na msaada, na Anapata heshima yote inapofanikiwa!

Imani inafungua mlango wa maisha ya ushindi! Kwa imani, tunaweza kweli kushinda dhambi kama Yesu alishinda! “"Huku ndio ushindi uushindao ulimwengu, yaani, imani yetu." 1 Yohana 5:5. Ninaamini katika uwezo wake wa kuniokoa kutokana na dhambi zote ninazojaribiwa. Ninaamini kwamba ninapochukua msalaba wangu na kusema Hapana kwa dhambi ninayojaribiwa, kama Yesu alivyofanya, nitashinda.

Biblia pia inaiita hii “Kusulubiwa Pamoja na Kristo”. “Nimesulubiwa Pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika Imani ya mwana wa Mungu, ambaye alinipenda na akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu.”  Wagalatia 2:20.

Imani ni kitu cha thamani sana kuwa nacho! Sio kitu tunachoweza kuona au kugusa, lakini Yesu alimwambia Tomaso mwenye shaka: “Wa heri wale wasioona, wakasadiki.”  Yohana 20:29. Petro pia anaandika: “Naye mwampenda, ijapokuwa hamkumwona, ambaye ijapokuwa hamwoni sasa, mnamwamini; na kufurahi sana, kwa furaha isiyoneneka, yenye utukufu, katika kuupokea mwisho wa imani yenu, yaani wokovu wa roho zenu.”  1 Petro 1:8-9.

Matokeo ya imani hii yanaweza kuonekana! Wanafunzi waliona kwa Yesu, na kama Wakristo tunapaswa kuja kwenye maisha haya ya furaha na utukufu - kwa imani!

Jamii
Chapisho hili linapatikana katika

Makala hii imejikita kwenye Makala ya Helen Simons awali ilichapishwa katika https://activechristianity.org/ na imechukuliwa na kupewa ruhusa kutumika kwenye tovuti hii.