Je, unasubiri muujiza?

Je, unasubiri muujiza?

Kutii kutatugharimu nini?

15/10/20155 dk

Na Ukristo wa Utendaji

Je, unasubiri muujiza?

Kutii kutatugharimu nini? Biblia inatuambia kuhusu miujiza mingi. Mungu alitenganisha Bahari ya Shamu, aliteremsha chakula kutoka mbinguni kwa ajili ya Waisraeli katika uhitaji wao na hata akamfufua Yesu kutoka kwa wafu!

Yesu pia alifanya miujiza mingi katika wakati wake. Aliponya vipofu na vilema, aligeuza maji kuwa divai nk.

Watu wengi wangekubali kwamba ingekuwa jambo la kustaajabisha kushuhudia mambo kama hayo.

Hebu fikiria kama ungelikuwa miongoni mwa Waisraeli ambao Musa aliwaongoza kutoka Misri. Umesimama katikati ya Bahari ya Shamu. Mungu ameigawanya mara mbili tu na unatembea kwenye ardhi kavu, yenye kuta ndefu za maji pande zote mbili unapopitia kuelekea kwenye usalama na uhuru.

Au vuta picha unaishi katika kijiji cha Bethania. Mtu mmoja aitwaye Lazaro, ambaye unamfahamu vizuri, amekufa kwa siku nne. Ulimsaidia kumbeba hadi kaburini mwake na kutazama jinsi familia yake ilivyokuwa ikiomboleza kwa ajili ya msiba wao. Lakini sasa, Yesu Kristo ametoka kumwambia atoke kaburini, naye yu hai tena! Anatembea kuelekea kwako, mzima na mwenye afya.

Unaweza kufikiria mwenyewe kwamba kwa hakika usingekuwa na shaka tena kama ungepitia miujiza kama hii.

Kulingana na ishara na maajabu

Hata hivyo, ndivyo hasa ilivyotokea watu wengi sana. Waliona na kushuhudia mambo ya ajabu kama hayo, lakini bado waliishia kuwa na mashaka. ( Zaburi 106:13; Yohana 12:37 ) Ni wachache tu walioamini kabisa kwamba Mungu angewatunza, hata baada ya kuwaonyesha mara kwa mara kwamba Angefanya hivyo. “Bwana akamwuliza Musa, Je! Watu hawa watanidharau hata lini? Wasiniamini hata lini? Nijapokuwa nimefanya ishara hizi zote kati yao.’” Hesabu 14:11.

Ni rahisi sana kwetu kutilia shaka. Tunategemea sana kile tunachokiona, kusikia na kuhisi. Matokeo yake ni kwamba mara nyingi tunamuuliza Mungu maswali au kuomba ishara au miujiza kabla ya kuchagua kumtii. Hapana shaka kwamba miujiza ilikuwa na sehemu muhimu katika historia yote. imefafanuliwa katika Neno la Mungu kama msaada kwetu kuamini, hata leo. ( Yohana 20:31 ) Lakini ni muhimu kujua kwamba miujiza yenyewe haiwezi kututosheleza kikamilifu. Miujiza inakusudiwa kujenga imani ndani yetu, na hilo ndilo jambo pekee litakalotutosheleza kwa kweli katika hali zote za maisha.





Imani hai

Tunahitaji kuwa na imani hai kwa Mungu! Imani kama hiyo ni zaidi ya kuamini tu kwamba kuna Mungu. Imani hai ina maana kwamba tunamtumaini Mungu katika kila hali, na kutafuta kufanya mapenzi Yake, haijalishi tunaona au kuhisi nini. Imani hai ina maana kwamba tunaamini katika Neno la Mungu na maneno ya manabii, Yesu Kristo na mitume, hata wakati ambao hakuna ishara za wazi au muujiza. Kimsingi, imani hai ni utii, hata wakati amabao hatuelewi mambo yote.

Ikiwa tunamwamini Mungu kweli, basi maisha yetu yanapaswa kuwa kitu kimoja na Neno lake. Neno la Mungu linaposema, “Msihangaike juu ya jambo lolote,” kwa mfano, hatupaswi kuketi na kuhangaikia pesa zetu au jinsi hali yetu inavyoweza kuonekana kuwa ngumu au isiyo na tumaini. Lakini pia hatupaswi kutarajia pesa kunyesha kutoka mbinguni. Hapana, tunahitaji kuwa watiifu kwa Neno la Mungu na kuyakataa mawazo yote ya kutotulia, wasiwasi na mashaka.

Vivyo hivyo, tunapokuwa katika hali ngumu, tunapohisi kupotea au kuchanganyikiwa, hatupaswi kutarajia kwamba Mungu atatokea na kurekebisha kila kitu kwa njia fulani ya kimuujiza. La, tunahitaji kufurahi, kama vile Petro aandikavyo katika 1 Petro 4:13 , na kuchagua kumshukuru Mungu kwa ajili ya majaribu tunayoyakabili, badala ya kulalamika au kuwa na uchungu. Tunahitaji kuamini kwamba Mungu atatumia kila hali kutubadilisha, hata wakati ambapo hatuelewi, au hisia zetu ziko chini kabisa. (Warumi 8:28.)

Matokeo

Matokeo ya imani na utiifu huo kwa Mungu ni kwamba tunakuwa wasioweza kutikisika. Tunamtumaini na kutafuta kufanya mapenzi yake na kisha anaweza kutenda mambo ya ajabu kati yetu. (Yoshua 3:5.) Lakini wale wenye mashaka, wale ambao hawako tayari kuamini na kutenda yale ambayo Mungu anasema katika Neno Lake, ni “…kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa hukuna huku ”. Yakobo 1:6. Watu wa namna hii hutegemea mambo ya nje; wanachanganyikiwa kwa urahisi na kukatishwa tamaa, na kwa sababu wana shaka, Mungu hawezi kuwasaidia katika maisha yao. ( Yakobo 1:6-7 )

Mungu hataki tutegemee ishara na miujiza ya nje, ambayo ni ya thamani kwa muda tu. Lakini imani na utii kwa Mungu ni wa thamani ya milele. Hivi ndivyo Mungu anataka kutoka kwetu: kwamba tumwamini yeye katika hali yoyote tuliyo nayo na kutafuta kufanya mapenzi yake bila kutarajia malipo yoyote ya kidunia. “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza, kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.” Waebrania 11:6.

Usisubiri ishara au muujiza. “ Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema Bwana wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.” Malaki 3:10. Ukifanya hivi, ukiamua kumwamini Mungu aliye hai na kulitii Neno lake, ukimpa maisha yako bila kuzuia chochote, hakika utapata baraka zake nyingi na nguvu kuu maishani mwako!

Chapisho hili linapatikana katika

Makala haya yanatokana na makala ya Nellie Owens yaliyochapishwa awali kwenye https://activechristianity.org/ na yamebadilishwa kwa ruhusa ya matumizi kwenye tovuti hii.