Mungu mwenye upendo anawezaje kuwapeleka watu jehenam?
Ni wazi kabisa kwamba jehanam ipo. Yesu anazungumza juu yake mara kadhaa katika injili. (Mathayo 23:33; Luka 12:5; Mathayo 16:18.) Lakini inaweza kuwa vigumu kufikiria jinsi Mungu mwenye upendo na rehema angeweza kuwapeleka watu mahali palipoelezewa kama "tanuru la moto". (Mathayo 13:50.)
Chaguo la mwisho – mambo mengine yote yanaposhindikana
Ndani ya mfumo wa haki, gereza mara nyingi huonekana kama chaguo la mwisho. Hii ni kwa sababu ya athari yake mbaya kwenye maisha ya mtu. Kwa kawaida, kadiri mhalifu anavyokaa gerezani, pamoja na wahalifu wengine, ndivyo uwezekano wa kuwa raia mwema tena unavyokuwa mdogo.
Lakini wakati mwingine ni chaguo pekee. Mbali na kuwa adhabu, katika hali zingine ndiyo njia pekee ya kuhakikisha kuwa hawatafanya uhalifu wowote zaidi.
Soma pia: Biblia inasema nini kuhusu Siku ya Hukumu?
Mungu mwenye rehema na mvumilivu
Inapohusu kuwahukumu watu jehanam , Biblia inaonyesha kama chaguo la mwisho la Mungu. " Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba." 2 Petro 3: 9.
Mungu hataki mtu yeyote atupwe jehanam. Anampenda kila mmoja ambaye amemweka duniani. Anawapa watu nafasi nyingi za kutubu na kupokea msamaha. Mungu huwafikia watu kwa njia nyingi tofauti, akifanya kazi ndani yao ili kupatamishwa naye. Hata alimtuma Mwanawe wa pekee duniani kutuonyesha njia, yote ili tupate kila fursa iwezekanayo kuokolewa. (Yohana 3:16.)
Katika siku za Nuhu " Bwana akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote." Mwanzo 6: 5 . Lakini Mungu alimwokoa Nuhu, na pamoja naye mustakabali wa wanadamu wote, baada ya kuamua kuharibu kila kiumbe hai. (Mwanzo 6.) Huu ni mfano wazi wa uvumilivu na rehema Zake.
Mungu ni yule yule leo. Chuki yake kwa dhambi na uharibifu unayosababisha haijapungua kwa muda. Vivyo hivyo na hamu yake ya dhati kwamba kila mtu atubu. Lakini Yeye hatamlazimisha mtu yeyote kutubu. Kila mmoja anahitaji kuamua kwa hiari yake mwenyewe kumtumikia Mungu badala ya kutenda dhambi.
Soma pia: Kwa nini Mungu alitupa uhuru wa kuchagua?
Yote huanza na hofu ya kimungu. Hofu ya Yusufu ya kutenda dhambi dhidi ya Mungu ilimruhusu aone dhambi jinsi Mungu anavyoiona na akasema: " Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?" Mwanzo 39: 9.
Ikiwa unafikiri kwamba kuhukumiwa kuzimu ni adhabu ngumu sana, basi huoni jinsi dhambi ilivyo mbaya. Mungu hawezi kuruhusu kitu chochote kichafu katika ufalme wake kwa sababu hicho kingeharibu kile kilicho kitakatifu na safi. Ikiwa dhambi ingekuja mbinguni, laana iliyo juu ya dunia kwa sababu ya dhambi pia ingekuja mbinguni, na Mungu hataruhusu hili kutokea. Sheria zake za milele, zisizobadilika zinasimama imara bila kutetereka, na Yeye hafanyi ubaguzi.
Jehanam sio mahali ambapo watu "wanapelekwa" tu. Kama vile kulivyo na njia inayoelekea mbinguni, pia kuna njia inayoelekea kuzimu. Ni njia ambayo watu wanaamua kupitia, mwelekeo wanaochagua muda mrefu kabla ya kufika huko. Mtu anapochagua kwa hiari kuishi kinyume na sheria za Mungu na kukataa kusikiliza Mungu anapomwambia atubu, yeye mwenyewe anachagua matokeo ya maisha yake yatakavyokuwa.
Mungu, Hakimu wa haki
" Atauhukumu ulimwengu kwa haki, Na mataifa kwa uaminifu wake.." Zaburi 96:13.
Hata watu ambao hawajawahi kusikia habari za Mungu, watahukumiwa na Yeye siku moja. Watahukumiwa kulingana na dhamiri zao, kulingana na hisia ya asili ya mema na mabaya ambayo kila mtu anayo, na jinsi alivyoishi kulingana nayo.
Mungu ni mwenye haki, na hakuna mtu atakayetupwa jehanam kwa kufanya kitu ambacho hakuelewa kilikuwa kibaya. Lakini mtu yeyote anayetenda kinyume na dhamiri yake siku moja atalazimika kuwajibika kwa hilo. (Warumi 2: 12-16.) Mungu ni mwadilifu sana kiasi kwamba hakuna mtu atakayeweza kusimama mbele yake siku hiyo na kusema kwamba haikuwa cha haki.
Kutoa hesabu ya maisha yako
Lakini hofu ya jehanam na hukumu ya milele haipaswi kuwa sababu kuu ya maamuzi yetu yote. Hapana, uvumilivu wa Mungu , rehema, na upendo wake kwetu unapaswa kuleta shahuku ndani yetu ya kumpenda yeye pia Kiasi kwamba tunaogopa kutenda dhambi dhidi yake. Jiulize tu, "Niko kwenye njia gani? Ni mawazo gani ninayoruhusu moyoni mwangu, na yatasababisha nini ikiwa nitayaweka moyoni mwangu?"
Chaguzi unazofanya sasa huamua ni wapi utakuwa milele, kwa hivyo usipuuze ukweli juu ya matokeo ya kutenda dhambi dhidi ya Mungu. Wakati wetu duniani utakapokwisha, kila mtu atalazimika kutoa hesabu mbele ya Hakimu wa haki . Siku hiyo, utasimama hapo, sio pamoja na marafiki au familia, lakini peke yako - wewe na Mungu tu. Huwezi kurudi nyuma na kuweka mambo sawa. Leo, bado unaweza.
Sasa ni wakati wa kuanza kwenye njia sahihi, njia isiyo na wasiwasi na kutotulia ambayo hutoka katika maisha ambayo hayako tayari kwa hukumu. Wale wote wanaochagua kutii sheria za Mungu zilizobarikiwa hupata uzoefu wa jinsi Yeye alivyo mwema! Wanaishi maisha kamili, wamejaa amani na furaha. Kila mahali watu kama hao wanaenda, wanaeneza furaha na nuru ya jua - bila kujali uchumi wao, afya, au hali nyingine za kibinafsi zilivyo. Kwa kuishi kulingana na amri za Mungu, kwa kweli huleta ladha ya mbinguni katika mazingira yao. Hivi ndivyo Mungu anavyotaka kwenye maisha yetu.