Tunaoneshaje upendo wetu kwa Mungu?

Tunaoneshaje upendo wetu kwa Mungu?

Mungu huoneshaje upendo wake kwetu? Na muhimu zaidi: Tunaonyeshaje upendo wetu kwa Mungu kwa kumjibu?

3/9/20263 dk

Tunaoneshaje upendo wetu kwa Mungu?

Upendo kamili hutoka pande zote mbili

Kawaida Watu hufikiri kwamba ikiwa mtu ana karama nyingi za kiroho, basi ni lazima Mungu ampende kweli. Lakini hili linaonyesha tu upendo wa Mungu kwetu, si upendo wetu kwake. Ushahidi pekee kwa Mungu kwamba tunampenda ni kwamba tunashika amri zake.

Wakati wa uamsho mara nyingi tunaona watu wakipokea karama nyingi za kiroho. Ungefikiri kwamba watu waliobarikiwa sana na Mungu wangempenda Mungu sana pia kwa kumjibu. Lakini kadiri miaka inavyopita, mara nyingi tunaona kwamba watu hawa hushindwa hata pale tendo dogo zaidi la utii linapohitajika kutoka kwao. Walikuwa na shauku maadamu walikuwa wakipokea karama—maadamu hakuna kitu kilichohitajika kutoka kwao.

Lakini mara tu Mungu anapoomba kitendo kidogo cha utii, wanakata tamaa kabisa. Je, hii ndiyo imani ambayo imejaribiwa na ni ya thamani kuliko dhahabu (1 Petro 1:7)? La! Ndiyo maana mtume anasema, “... Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake..” 1 Yohana 2:5. Tafsiri nyingine inasema: “Lakini wale wanaolitii neno la Mungu huonyesha kweli jinsi wanavyompenda kikamilifu.”  

Ikiwa upendo unatoka upande mmoja tu, si upendo mkamilifu. Ili uwe mkamilifu, lazima utoke pande zote mbili. Na ndipo tu tunaweza kusema kwamba tuko ndani yake na yeye yuko ndani yetu (1 Yohana 3:24).  

Upendo wa Mungu hukamilika tunapoishi katika ushirika pamoja na Baba na Mwana

Amri ya kupenda hubaki kuwa amri ya zamani upendo huu unapotoka tu upande wa Mungu. Lakini tukizishika amri Zake, amri ya zamani itakuwa amri mpya iliyo kweli ndani yetu pia, kama vile ilivyo kweli ndani Yake. Upendo huu kutoka kwa Mungu kwetu na kutoka kwetu kwa Mungu utaiondoa giza, na nuru ya kweli itaangaza kwa nguvu zake zote.

Neno la kinabii ni kama nuru inayong’aa mahali penye giza (2 Petro 1:19). Neno la kinabii ni amri takatifu (2 Petro 2:21). Tukizishika amri za Mungu, mahali hapa penye giza katika moyo wetu patatiwa nuru. Kila kitu kilichokuwa nuru na kweli ndani yake kitakuwa nuru na kweli ndani yetu. Tukiendelea kutii amri takatifu, mchana utakucha na nyota ya asubuhi itaangaza mioyoni mwetu, kama inavyosema katika 2 Petro 1:19.

“Hilo tuliloliona na kulisikia, twawahubiri na ninyi; ili nanyi pia mpate kushirikiana nasi: na ushirika wetu ni pamoja na Baba, na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo. Na haya twayaandika, ili furaha yetu itimizwe.” 1 Yohana 1:3-4.

Haiwezekani kuwa na ushirika pamoja na Baba na Mwana bila kuzishika amri za Mungu. Na bila hili, furaha yetu pia haitakamilika.

Kuzishika amri za Mungu

 Watu hujidanganya wenyewe wanapoishi maisha yasiyo na maana na hawamwulizi kamwe Mungu mapenzi Yake kwao ni yapi! Wanapenda kufikiria kuhusu siku walipookolewa au kubatizwa katika Roho na kupokea karama ya kunena kwa lugha. Lakini mtume Paulo alisahau yale yaliyokuwa nyuma na akakimbilia yale yaliyokuwa mbele.

Tukitaka kufanya maendeleo katika ufalme wa Mungu katika siku zijazo, tunahitaji kujifunza amri za Mungu ni zipi, kujua mapenzi yake na kujitoa wenyewe katika nguvu ya Roho. Kwa njia hii tutakua katika Bwana. Na wale waliodhani kwamba mnaishi katika utumwa watashangaa sana watakapotambua kwamba njia hii ambayo waliidharau, kwa kweli ndiyo njia ya Mungu.

Chapisho hili linapatikana katika

Makala hii imetafsiriwa kutoka Kinorwe, na ilichapishwa kwanza chini ya kichwa “Amri za Kale na Mpya” katika jarida la BCC “Skjulte Skatter” (“Hazina Zilizofichwa”) mwaka 1922. Imebadilishwa kwa idhini kwa ajili ya kutumiwa katika tovuti hii.

Hakimilikii © Stiftelsen Skjulte Skatters Forlag