Ushindani unaweza kuwa jambo kubwa kwa vijana (na labda kwa wazee pia). Kuwa "bora zaidi". Kuwa na utani wa kuchekesha zaidi, kufunga magoli mengi zaidi, kuwa na elimu kubwa zaidi, nk. Wanataka kuwa bora zaidi katika kila jambo wanalolifanya. Ni njia ipi sahihi ya kuchukulia hili kama Mkristo ambaye anataka kuishi kwa moyo wote kwa ajili ya Mungu?
Unashindania nini?
Sio jambo baya kuwa na ushindani. Ni vizuri kujiwekea malengo, kufanya uwezavyo, au kuwa na mashindano ya kirafiki ili kujipa changamoto.
Lakini jipime mwenyewe. Kwa nini unafanya hivyo? Kwa sababu ya kiburi, au wivu, au uchoyo, au ubinafsi? Kwa sababu unajali sana watu wanafikiria nini kukuhusu? Hakikisha kwamba matendo yako hayatawaliwi na tamaa za dhambi! Tunapofanya kazi kwa bidii ili kuwa bora zaidi, je, ni lazima tuwakanyage wengine ili tufanikiwe ? Kama ilivyo katika mambo mengine yote , tunahitaji kuchunguza kama kuna dhambi nyuma ya matendo yetu, na ikiwa ipo, tunapaswa kujitakasa na kuiondoa
" Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu,." Wakolosai 3:12.
Kwa nini kila kitu kinapaswa kuwa mashindano?
Mara nyingi, hitaji la kushindana hutokana na hisia ya kutokuwa bora vya kutosha. Tunataka kujithibitishia, angalau kwetu wenyewe, kwamba sisi ni bora katika jambo fulani ili kuhisi kama tuna thamani. Sababu nyingine inaweza kuwa kiburi.
Ukweli ni kwamba kuna jambo moja tu ambalo tunapaswa kuthibitisha maishani, na hilo ni kwamba tunampenda Kristo kwa moyo wetu wote. " Katika hayo ninyi nanyi mlitembea zamani, mlipoishi katika hayo. Lakini sasa yawekeni mbali nanyi haya yote, hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi vinywani mwenu." Wafilipi 3: 7-8.
Je, tunaweza kujifunza kuona vitu vyote - ikiwa ni pamoja na jina letu zuri, jinsi watu wanavyotuona, ubinafsi wetu – kama havina thamani na takataka ikilinganishwa na ukuu wa kumjua Kristo? Ni nini kinachoweza kuwa na thamani zaidi kuliko hilo?
Usiruhusu dhambi ikushinikize. Huna haja ya "kuwa" mtu yeyote. Sio muhimu watu wanafikiria nini juu yako kulingana na jinsi ulivyo mzuri na ulivyofanikiwa. Kilicho muhimu ni kwamba tunaweza kusimama mbele ya uso wa Mungu na kujua kwamba hatuna dhambi kwenye dhamiri zetu. Kwamba sisi ni safi na hatuna lawama. Hiyo itatupa thamani ya kweli katika ufalme wa mbinguni.
" Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa." Mathayo 23:12.
Chaguo jingine ni nini?
Hapa kuna chaguo la Kibiblia ambalo linafaa kushindania:
" Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga mbio, hupiga mbio wote, lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate. Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote; basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika." 1 Wakorintho 9: 24-25.
Unaona taji hiyo ambayo itadumu milele kama kitu cha kushinda kwa gharama yoyote? Fanya mambo yote kutoka moyoni mwako kama kwa Bwana, kwa njia ambayo hairuhusu kiburi, ubinafsi n.k kuishi! Tafuta mahali ambapo umejaa kiburi, na ushinde hilo na badala yake utafute mema ya mwingine. Tafuta kuwa bora katika mambo ambayo ni muhimu sana. Tafuta kuwa "bora" katika kuwa mnyenyekevu wa moyo. Fanya yote unayofanya ili Mungu atukuzwe na dhambi ishindwe.
Je, haingeshangaza ikiwa tungeshindana katika kuwa na matunda mengi ya Roho? Kuwa mnyenyekevu zaidi, asiye na ubinafsi zaidi, nk? Huo ungekuwa ulimwengu ulioje, na kila mtu akishindana zaidi kuwa kama Kristo!
" Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine." Wafilipi 2: 3-4.
Utawezaje kuishi hivyo?
Utafikia tu maisha kama hayo kwa kumwomba Mungu akuonyeshe mahali unapoishi kwa ajili yako mwenyewe, ambapo kuna dhambi nyuma ya kile unachofanya. Unaposoma Neno la Mungu anaweza kukuonyesha njia sahihi ya kufanya mambo, ili uweze kuelewa mapenzi Yake na kuishi kulingana nayo. Kwa kuwa mwaminifu katika nia yako, kukubali ukweli juu yako mwenyewe, kuhukumu dhambi kwa jinsi ilivyo, kuchukia udhalimu na kuishinda. Kwa kufanyia mazoezi kwa uangalifu mistari hiyo katika Wafilipi katika maisha yako.
Matokeo ni nini?
Ambapo matendo yako hapo awali yaliathiriwa na kiburi na ubinafsi, sasa unaweza kuwatumikia na kuwabariki wengine. Hazina yako iko mbinguni badala ya vitu vya nchi; na ukosefu wako wa kujiamini, na hisia hizo zote hasi hauzijali tena unapolinganisha na jinsi unavyokuwa, unakuwa mtoto wa Mungu, umejiandaa kikamilifu kwa matendo mema. (2 Timotheo 3:17.)
Kisha watu watapata wema wa Kristo kutoka katika maisha yako. Unakuwa nuru katika ulimwengu huu. Unaweza kufanya yote unayofanya, bila kiburi na ubinafsi! Utu wako unasafishwa kutoka kwa dhambi na unaweza kufanya kila kitu kwa roho nzuri, na matokeo mazuri ambayo hujenga ushirika na kuunda uhusiano uliobarikiwa, safi na wengine bila maslahi ya kibinafsi kuingia kati yako.