Imani hai

Imani hai

Watu wengi hushindwa kuwa huru kutoka katika maisha yao ya zamani, lakini kwa imani iliyo hai kwa Mungu inawezekana kutoelemewa tena na mambo ya zamani

2/7/20252 dk

Written by Kaare J. Smith

Imani hai

3 dak

Kuwa huru kutoka mambo ya zamani

"Msiyakumbuke mambo ya kwanza, wala msiyatafakari mambo ya zamani. Tazama, nitatenda neno jipya; sasa litachipuka; je! Hamtalijua sasa? Nitafanya njia hata jangwani, na mito ya maji nyikani." Isaya 43: 18-19.

Ni utukufu kutazamia siku zijazo. Hatupaswi kusumbuliwa na mambo yaliyo nyuma yetu ikiwa tumeweka mambo sawa na Mungu na watu ambapo hilo lilikuwa jambo muhimu. Kisha hatupaswi kufikiria juu ya kile kilichotokea hapo awali, au juu ya kilichopita. "Tazama jambo jipya nitakalofanya," Anasema.

Watu wengi hawawezi kuwa huru kabisa kutoka katika maisha yao ya zamani. Lakini inasema katika Isaya 53:5, "... Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.." Mtu anaposumbuliwa na kukata tamaa kila wakati, kuna sababu moja tu ya hilo; Hana imani hai kwamba dhambi zake zimesamehewa, haamini kabisa.

Tunapaswa kupata imani iliyo hai!

Unawezaje kuvunjika moyo ikiwa unaamini kwamba dhambi zako zimeondolewa kutoka kwako kama mashariki ilivyo mbali na magharibi? (Zaburi 103:12.) Je, unaliamini hili kweli? Kisha kuvunjika moyo kutakuwa jambo la zamani. Shukrani na sifa kwa Mungu! Je, kweli unaamini kwamba Yeye amezitupa dhambi zako katika bahari ya usahaulifu (Mika 7:19), na kwamba hutaziona tena? Fikiria juu ya hili, wewe unayesoma hili!  Pokea imani iliyo hai ndani yake! Omba kwa Mungu akujaze roho ya imani! Nini kitatokea kwa kukata tamaa basi? Itatoweka kabisa!

Lazima tufikie imani iliyo hai katika msamaha wa dhambi, huo ndio msingi wa lengo kuu, ambalo ni uzima mtukufu, wa kushinda katika Yesu Kristo. Lengo letu ni kujazwa na utimilifu wote wa Mungu—kwa hekima, wema na rehema—kwa njia ambayo wengine wanaweza kuiona ndani yetu. (Yakobo 3:13.) Haya ni maisha ya utukufu!

Hii inahusiana na maisha yetu ya ndani. Sio tu juu ya kushika sheria zote ambazo Musa alitoa. Hapana, tunapaswa kufunua amri za Yesu ambazo ameandika katika mioyo na akili zetu, na tunafunua nguvu tunayopokea kuzitii - kupitia neema iliyo ndani ya Yesu Kristo. Hii ni kazi ya neema.

Makala hii imetafsiriwa kutoka Kinorwe na ni dondoo kutoka kwenye kitabu "Mchungaji na Nabii," (Skjulte Skatters Forlag, 2004) cha Kaare J. Smith. Imebadilishwa kwa ruhusa ya matumizi kwenye tovuti hii.

Shiriki