Wokovu baada ya kupatanishwa
Baada ya kuokolewa, kuna zaidi ambayo Mungu anataka kutuokoa nayo. Warumi 5:10 inasema, “Kwa kuwa kama tulipokuwa adui wa Mungu tulipatanishwa naye kupitia kwa kifo cha Mwanawe, si zaidi sana baada ya kupatanishwa, tutaokolewa kwa uzima wake.”
Katika wokovu wa kwanza tunapokea msamaha wa dhambi tulizotenda, na tunapatanishwa na Mungu, tunapata amani na Mungu. Wokovu wa pili huja kwa kutembea katika utii wa imani (Warumi 1:5), kwa sababu imeandikwa: Tembeeni katika nuru ilhali mna nuru, ili mpate kuwa watoto wa nuru (Yohana 12:36). Katika nuru kuna uzima, na uzima ndio nuru ya wanadamu (Yohana 1:4). Kuwa mtoto wa nuru ni sawa na kuwa mtoto wa uzima. Yesu Kristo ni mkuu wa nuru; Yeye ni mkuu wa uzima, kama vile Shetani alivyo mkuu wa giza; yeye ana nguvu ya mauti.
Kufanywa hai na Roho
Wokovu unaopatikana kupitia maisha ya Kristo ni kwamba, kwa Roho wake na kupitia nuru na uzima wake, hufanya roho yetu kuwa hai. Katika Yakobo 4:5-6 imeandikwa kwamba Mungu huitamani kwa wivu roho aliyoitia ndani yetu, lakini neema anayoitoa ni zaidi sana. Nuru inavyoongezeka, ndivyo giza linavyopungua. Nuru huleta uzima, na giza linapotoweka, kifo nacho huondoka, na yule aliyekuwa na nguvu za mauti—shetani—basi naye huharibiwa.
Mtume Paulo bado alikuwa hajafikia wokovu kamili kupitia uzima wa Kristo, bali alifanya kila juhudi kuuifikia (Wafilipi 3:12). Ni lazima na sisi pia tufanye kila juhudi kuufikia mwisho huu katika wokovu huu. Ni mwisho ulio juu sana ndani ya sheria kamili ya uhuru (Yakobo 1:25).
Katika wokovu wa kwanza, Yesu alijitoa mwenyewe kuwa sadaka kwa ajili ya dhambi zetu. Katika wokovu wa pili, Yeye ni Kuhani wetu Mkuu na Mtetezi wetu. Yeye ndiye Mpatanishi wa agano jipya. Hii ina maana kwamba anasimama kati ya Mungu na sisi, baada ya kulipa kwa kifo chake kwa ajili ya dhambi ambazo watu walitenda chini ya agano la kwanza (Waebrania 9:15).
Hukumu huleta wokovu
Petro pia anazungumza juu ya wokovu kupitia maisha ya Kristo katika 1 Petro 4:17-18: “Kwa maana wakati umewadia wa hukumu kuanzia katika nyumba ya Mungu. Basi ikianzia kwetu sisi, mwisho wa hao wasiotii Injili ya Mungu utakuwaje? Basi, ‘Ikiwa ni vigumu kwa mwenye haki kuokoka, itakuwaje kwa mtu asiyemcha Mungu na mwenye dhambi?’”
Hukumu huanza katika nyumba ya Mungu, yaani, pamoja nasi. “Na hii ndiyo hukumu: nuru imekuja ulimwenguni.” Yohana 3:19. Tunapata hukumu hii Mungu anapomulika nuru yake juu yetu. Katika nuru hii tunatambua kwamba ni lazima tupange mambo sawasawa. Hiyo ndiyo njia pekee tunaweza kuwa waaminifu kwa nuru na kuwa watoto wa nuru. Na kwa sababu tu nuru inaleta hukumu, watu huichukia.
Ikiwa kila kitu katika moyo wa mtu kingekuwa katika mpangilio mkamilifu, nuru ingemletea furaha kuu, naye angeifurahia nuru. Lakini kwa asili sisi ni waovu; sisi ni giza tupu na tumefanya kazi nyingi za giza zinazohitaji kusafishwa kwa njia ya nuru na hukumu. Kwa hiyo nuru hutuhuzunisha badala ya kutufurahisha. Yule mtawala kijana tajiri aliondoka akiwa na huzuni, na watu wengi leo hufanya vivyo hivyo wakati nuru ya Neno inaangaza mioyoni mwao. Maandiko yalijua hili, na ndio sababu imeandikwa, “Leo, mkiisikia sauti yake, msiifanye mioyo yenu migumu.” Waebrania 3:7-8.
Wokovu kwa uzima wa Kristo
Itakuwaje ikiwa hatutafanya mioyo yetu kuwa migumu? Ndipo tutakwenda kutoka nuru hadi nuru zaidi. Tunakuja kuelewa kwamba hukumu huongoza kwenye haki, na hatuogopi sana kujihukumu wenyewe na kukubaliana na nuru. Hili hutokea kwa urahisi zaidi na zaidi kwetu, kwa sababu tunapoendelea kutembea katika nuru, tunaona kwa uwazi zaidi jinsi tulivyo maskini kulingana na mwili wetu wa dhambi. Hili hutupa chuki kubwa kwa maisha yetu ya kibinafsi na hutusaidia kupita mtihani ambao Kristo anawahitaji wale wanaotaka kuwa wanafunzi wake.
Utukufu utaongezeka kwa sababu mateso katika mwili huweka giza na uovu chini ya udhibiti. Tunazidi kufahamu urithi wetu katika nuru (Wakolosai 1:12). Ushirika wa kindugu hukua na kuwa na joto zaidi. Damu husafisha dhambi zote, na ukaribu wetu na ushirika wetu na Baba unakuwa mkuu kuliko hapo awali. Huduma yetu katika Roho inakuwa yenye thamani zaidi, na watu wengi zaidi watatuchukia na kulikataa jina letu kuwa baya.
Yesu alisikiwa kwa sababu ya kumcha Mungu kwake (Waebrania 5:7). Kwa kutembea katika nuru, tunaonyesha kwamba kweli tunamcha Mungu, na Mungu ataweza zaidi kusikia maombi yetu. Mambo haya yote ni sehemu ya wokovu unaokuja kupitia uzima wa Kristo. Na wokovu huu unaweza tu kuanza kutenda kazi baada ya kifo kutokea ili kutuokoa kutoka kwa dhambi tulizotenda chini ya agano la kwanza.