Mwana wa Mungu ni mkuu kiasi gani?

Mwana wa Mungu ni mkuu kiasi gani?

Je, umewahi kufikiria kuhusu Yesu, Mwana wa pekee wa Mungu, na kile Alichofanya ili tuwe ndugu zake?

13/3/20253 dk

Na Ukristo wa Utendaji

Mwana wa Mungu ni mkuu kiasi gani?

Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu. Yeye kwa kuwa ni mng'ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake, akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu.” Waebrania 1:1-3.

Mwana wa pekee wa Mungu

Hivyo ndivyo alivyo mkuu, Yeye ni Mwana wa pekee wa Mungu. "Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele." Yohana 3:16.

Ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu.”. Wafilipi 2:6-7.

Yesu, ambaye alikuwa Mwana wa Mungu na mrithi wake wa pekee, aliacha kuwa sawa na Mungu. Alitaka kuwa na ndugu ambao pia walikuwa wamepata asili ya kimungu na ambao wangeweza kurithi pamoja Naye. Lengo   lilikuwa ni kutupa uwezekano huu, wokovu huu, ndio maana Yesu alikuja duniani. Na alipokwisha kumaliza kazi, imeandikwa hivi kuhusu yeye: “Hata tena, amletapo mzaliwa wa kwanza ulimwenguni, asema, Na wamsujudu malaika wote wa Mungu.” Waebrania 1:6

Imeandikwa zaidi kuhusu Mwana wa Mungu: “Kiti chako cha enzi, Ee Mungu, ni cha milele na milele… Umependa haki na umechukia maasi; kwa hiyo Mungu wako amekutia mafuta, mafuta ya shangwe kupita wenzio.” Waebrania 1:8-9.

Yeye ni mzaliwa wa kwanza - na inawezekana kwetu kuwa kaka na dada zake!

Tunaona kwamba ana wenzake, katika tafsiri nyingine ya Biblia imeandikwa kwamba ana ndugu, lakini ni mzaliwa wa kwanza; Yeye ndiye aliyemaliza kazi na kutupa uwezekano wa kuwa ndugu zake kweli. Yesu aliona hilo kuwa jambo kuu sana kwa sababu mara tu Alipofufuka kutoka kwa wafu, Alisema: “Lakini enenda kwa ndugu zangu ukawaambie, ‘Ninapaa kwenda kwa Baba yangu naye ni Baba yenu, kwa Mungu wangu naye ni Mungu wenu.’” Yohana 20:17.

Tunasoma jinsi alivyofurahi sana kuwa na ndugu. “Anasema, “Nitalihubiri jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kanisa nitakuimbia sifa.” Waebrania 2:12. Tunaweza pia kusoma juu ya ahadi za ajabu anazowapa ndugu zake: “Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda, nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi. Ufunuo 3:21.

Lakini sasa swali ni: je, tunaona kwa ukubwa ukweli kwamba sisi ni kaka na dada zake kama vile Yeye anavyoona, kwamba tutaacha kila kitu ili kumpata Kristo? Yohana anaandika jambo ambalo ni la maana sana: “Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu;.” 1 Yohana 3:1.

Hili sio jambo ambalo tumeitiwa tu, lakini ni kweli kabisa. Tunaposoma: "Yeye ashindaye ... kama mimi nilivyoshinda." Ni lazima kweli tuwe ndugu zake. " Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye." 1 Yohana 3:1. Ikiwa tuna uthibitisho huu, tunaweza kuwa na furaha tele.

Makala hii ni sehemu ya kitabu “So Great a Salvation”, iliyoandikwa na Sigurd Bratlie na kuchapishwa na Skjulte Skatters Forlag (Hidden Treasure Publications) mwaka wa 1982. Imetafsiriwa kutoka katika Kinorwe na imechukuliwa kwa ruhusa ya kutumika kwenye tovuti hii.

Shiriki