Bila hila wala unafiki!
“Basi Yesu akamwona Nathanaeli anakuja kwake, akanena habari zake, Tazama, Mwisraeli kweli kweli, hamna hila ndani yake. Nathanaeli akamwambia, Umepataje kunitambua? Yesu akajibu, akamwambia, Kabla Filipo hajakuita, ulipokuwapo chini ya mtini nilikuona..'” Yohana 1:47-48.
Karibuni Yesu atakuja tena, na Waisraeli wote wa kweli wa kiroho ambao hamna hila wala uongo ndani yao, watanyakuliwa.
Yesu alikuwa huru kabisa kutoka katika kila aina ya uongo na unafiki. Dhabihu yake ilikuwa ya moyo wote na ya dhati, na ilimgharimu damu yake. Lakini kila alipokwenda, alikutana na hila na unafiki wa kidini. Walimheshimu Mungu kwa midomo yao, lakini mioyo yao ilikuwa mbali naye.
“Wakati huo huo, watu wengi sana walipokuwa wamekusanyika hata wakakanyagana, alianza kuwaambia wanafunzi wake kwanza, Jihadharini na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.’” Luka 12:1.
Hapa tunaweza kuona jinsi Yesu alivyouchukulia kwa uzito unafiki. Aliuchukia! Kwa hiyo tunaweza kuelewa ni kwa nini Yesu alifurahi sana alipomkuta Nathanaeli. Yesu hakumpa ushuhuda wa juujuu tu. Alikuwa amemchunguza kwa karibu alipomwona chini ya mti.
Wawazi na waaminifu, wakiwa na maisha yao katika nuru
Yesu anaweza kutoa ushuhuda huu huo kwa Waisraeli wote wa kiroho—wale ambao ni sehemu ya bibi arusi Wake. Je, anaweza kusema hivi kuhusu mimi na wewe tunapofanya kazi zetu za kila siku? “Tazama, Mwisraeli wa kweli, ambaye hamna hila ndani yake!” Ikiwa sivyo, basi tunapaswa kuhakikisha kwamba anaweza kusema hivi juu yetu haraka iwezekanavyo, ili tuweze kufanywa wakamilifu na kuwa tayari kwa kuja Kwake.
Sharti la kukubaliwa katika shule ya wanafunzi wa Yesu ni kuacha kila kitu, na kuvua hila na unafiki wote na uovu wote (1 Petro 2:1; Yakobo 1:21).
Ni vizuri sana kuwa pamoja na wanafunzi wa kweli kama hawa, tukijua kwamba hatutakutana kamwe na chochote kibaya kikitoka kwao. Hawana nia za siri kamwe. Wako wazi na waaminifu; maisha yao yako katika nuru. Hufikiri, huzungumza, na kutenda mema. Kamwe hatuwi na lolote jingine kutoka kwao. Tungeweza kama kuangalia mioyo yao, tungeikuta hata zaidi mema kuliko yale tunayoweza kuona nje. Huu ndio udugu wa kweli, wa dhati katika mwili wa Kristo. Hubaki imara katika siku nzuri na mbaya hapa duniani, na milele yote.
Itakuwa siku kuu Yesu atakaporudi kuwachukua “wanafunzi” Wake waliotamani kujifunza na ambao Yeye Mwenyewe amewafundisha kikamilifu, kwa sifa na utukufu Wake wa milele. Watakuwa mawe ya milele katika Yerusalemu mpya, na mataifa yatatembea katika nuru na utukufu wake (Ufunuo 21). Utukufu huu ni wa kweli kabisa.
Uweke moyo wako safi
Injili ni nguvu halisi ya kutuokoa kutoka katika kila aina ya hila na unafiki. Petro alihubiri injili, na mioyo ya Mataifa ikatakaswa kwa imani (Matendo 15:9). “Heri walio na moyo safi, maana hao watamwona Mungu. Heri wenye moyo safi; Maana hao watamwona Mungu.” Mathayo 5:8. Lakini kuutunza moyo wetu uwe safi hakutokei kiotomatiki. “Zaidi ya yote, linda moyo wako, kuliko yote uyalindayo, maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.” Mithali 4:23.
Vishawishi huja kama mawazo mabaya na machafu kutoka katika mwili wangu na hutaka kupata nafasi moyoni mwangu. Hapa ndipo ninahitaji kupigana kwa imani ili kuutunza moyo wangu uwe safi. Si dhambi kujaribiwa, lakini nikifungua moyo wangu kwa mawazo mabaya na machafu, basi nitakuwa mwovu na mchafu. Hatupaswi kumwacha shetani atushinde. Ni lazima tupinge, tukiwa thabiti katika imani. Ni lazima tuzime mishale yote yenye moto ya yule mwovu kwa ngao ya imani (Waefeso 6:16).
Kwa imani katika Kristo, inawezekana kweli kuutunza moyo wetu uwe safi, bila hila wala unafiki, hata katika siku hizi za mwisho za uovu wakati watu wana mfano wa utauwa, lakini wanakana nguvu zake (2 Timotheo 3:5).
Roho thabiti
“Hakika wewe wapendezwa na kweli inayotoka moyoni; wanifundisha hekima ndani ya moyo wangu.” Zaburi 51:6. Ikiwa Mungu hana nafasi katika sehemu ya ndani kabisa na ya kina kabisa ya moyo wangu, hawezi kunipa kile anachokithamini zaidi—hekima yake, ambayo kuliko yote ni safi. “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho ya uthabiti ndani yangu.” Zaburi 51:10.
Roho hii si ya kuyumba-yumba, kutikisika, au kubadilika-badilika, bali ni thabiti na ya kuaminika – roho ambayo wote Mungu na watu wanaweza kutegemea katika kila lililo tukufu, jema, na la kweli. Hawa ndio aina ya ndugu alio nao Yesu, ambao pamoja nao atafurahi milele katika utukufu mkuu kuliko wote. Na Yesu ndiye mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu kama hao (Warumi 8:29).