Kama wengi wetu, nimejaribiwa kwa mawazo ya giza na mazito maishani mwangu: mawazo ya kujihurumia na kutofurahishwa na hali yangu. Lakini, pia nimegundua kwamba Mungu na Neno lake ni kweli katika maisha yangu.
Mungu amenipa vitu vingi sana. Nina kazi nzuri, mahali pazuri pa kukaa na marafiki wema. Nina mambo mengi ya kushukuru.
Kujaribiwa kuwa na wasiwasi
Lakini ninaishi mahali ambapo mara nyingi ni baridi, na anga ni kijivu. Wakati mwingine, huhisi kama inanilemea, pamoja na shinikizo nyingine zote ninazopitia katika maisha yangu - bili ninazopaswa kulipa, siku ngumu za kazi, na kila aina ya wasiwasi mwingine. Inashangaza ni mambo mangapi nadhani yanapaswa kuwa tofauti: hali ya hewa inapaswa kuwa tofauti, ninapaswa kuwa na kazi bora zaidi, na kwa nini bado sijaoa? Ni rahisi kujisikia huzuni na kutokuwa na furaha.
Lakini kuna habari njema! Ninapopata mawazo haya mazito kuhusu maisha yangu, na ninapofikiria maisha yanapaswa kuwa tofauti kuliko yalivyo, si lazima nikubali mawazo hayo. Kwanza kabisa, mimi ni mwanafunzi wa Yesu Kristo. Nimemkabidhi Mungu maisha yangu yote—kila kitu nilicho nacho. Na mimi napata nini kwa kufanya hivyo? Kila kitu. Sina sababu ya kuwa na wasiwasi.
Yesu ametuambia, “Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” Mathayo 11:30 (NLT). Hapo awali, anasema, “Bali utafuteni kwanza ufalme wa Mungu na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” Mathayo 6:33 (NLT). Ninapotafuta Mungu kabla ya kitu kingine chochote, atahakikisha kwamba nina kile ninachohitaji katika maisha yangu na maendeleo yangu ya kiroho.
Kwa hakika, hii si njia ya kawaida ya kufikiri. Ni kawaida kulalamika, kufikiri kwamba labda Mungu alikosea mambo na kwamba maisha yangu yanapaswa kuwa tofauti. Lazima nipigane dhidi ya yale ambayo mwili wangu na hisia zangu zinataka kufanya, na nyakati nyingine ni vigumu sana. Lazima niombe tena na tena, “Mungu, nisaidie kuwa mwaminifu! Nisaidie kushukuru kwa kila jambo!”
Kisha nahitaji tu kuamini na kutii amri ya Mungu inaposema, “msijisumbue kwa jambo lolote”!” Wafilipi 4:6. Iwapo naamini kwamba Mungu ananitakia mema katika siku nzuri, je, si kweli vivyo hivyo katika siku mbaya?
Mungu anajua ninachohitaji
Siwezi kamwe kuhitaji kukubali hisia hizo nzito na za giza za kujihurumia, za kutokuwa na furaha. Watu wengi sana wanatatizwa na mambo haya, lakini mimi si lazima nitatizwe nayo. Kwa nini? Kwa sababu naamini kwamba maisha yangu hayaishii ninapokufa, bali nitaishi tena, mbinguni. Ninaamini kwamba maisha hapa ni wakati wa mafunzo kwa ajili ya umilele - kwamba ninaandaliwa kwa ajili ya mbingu. Kila wakati ninaposaidiwa na nguvu za Roho Mtakatifu kusema Hapana kwa hisia hizo za wasiwasi na kutokuwa na utulivu, ninakuwa hatua moja karibu zaidi ya kuachiliwa huru nazo milele. Na nilichogundua ni shukrani ya kina na ya kweli moyoni mwangu kwa kila jambo.
Huenda ikaonekana kuwa jambo la ajabu, lakini hali zinazoonekana kuwa nzito na zisizo za haki zimenifanya nimshukuru Mungu, kwa sababu ninaweza kuona kwamba kweli ni kwa manufaa yangu.
Mungu anajua ninachohitaji na naweza kushuhudia hili: Ukimpa Mungu kila kitu, atakulipa kila kitu. Huenda si kila kitu unachotaka, bali itakuwa kila kitu unachohitaji. Maisha haya ninayoishi kama mwanafunzi wa Yesu yananifanya nifurahi zaidi kuliko ninavyoweza kueleza kwa maneno. Ni furaha ya kweli, halisi kuishi hivi.