Mahali ambapo Mungu hufanya makao yake

Mahali ambapo Mungu hufanya makao yake

Mungu anataka kuwa na roho yetu, na anataka kufanya makao yake ndani yetu tena. Anafanyaje hili?

24/9/20184 dk

Na Ukristo wa Utendaji

Mahali ambapo Mungu hufanya makao yake

Tangu Anguko Shetani alipofanya makao yake miongoni mwa watu duniani, Mungu amejaribu kujitafutia makao katika mioyo ya wanadamu. Ameweza kupata nafasi katika nafsi chache zinazomcha Mungu hapa na pale, lakini si sana, kwa sababu ya dhambi zote zinazoishi katika asili ya watu. Paulo aliwaandikia Wakorintho akiwaomba wakunjue mioyo yao kwa sababu walikuwa hakuna nafasi ndani yao. Aliona vigumu kupata nafasi katika mioyo yao. ( 2 Wakorintho 6:11-13 )

Mahali pa Mungu pa kuishi

Ni kazi ya Roho wa Mungu kwamba "tunajengwa" ili kuwa mahali ambapo Mungu anaweza kuishi, kama ilivyoandikwa katika Waefeso 2:19-22: "Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji Pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu. Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kuku ahata liwe hekalu takatifu katika Bwana. Katika yeye ninyi nanyi mmejengwa Pamoja kuwa maskani ya Mungu katika roho.”

Tunaona kwamba kila mmoja wetu ni nyumba ambayo Mungu anaishi kwa njia ya Roho Wake, na kwamba tunakua pamoja na wengine kuwa hekalu ambalo limetolewa wakfu kwa Bwana. Mtu anaweza kuona wazi kwamba watu hawa ambao ni makao ya Mungu wameunganishwa, wawe pamoja au wametengana.

Au mwadhani kwamba maandiko yasema bure? Huyo roho akaaye ndani yetu hututamani kiasi cha kuona wivu? Lakini hutusaidia sisi neema iliyozidi…” Yakobo 4:5-6.

Kama matokeo ya Anguko, Shetani aliipotosha roho ambayo Mungu alipuliza ndani ya Adamu, na dhambi ikaja katika mwili, nafsi, na roho ya watu wote. Roho yetu ya kibinadamu pia ilikuja chini ya sheria ya dhambi na kifo. Lakini Mungu anataka kumiliki roho zetu. Kwa hiyo, anatupa neema nyingi katika vita vyetu vya kuwa huru kutoka kwa nguvu na udhibiti wa Shetani. (Soma Waroma 8:2.)

Kufanywa hai katika roho

Imeandikwa kwamba Adamu wa mwisho ni Roho yenye kuhuisha. (1 Wakorintho 15:45.) Adamu wa mwisho ni Yesu Kristo, na ndiye atendaye kazi ndani yetu. Roho yetu ya kibinadamu iko chini ya sheria ya dhambi na mauti na Yesu amepewa kazi ya kuzifanya roho zetu kuwa hai.

Katika 1 Petro 3:18 imeandikwa kwamba "Mwili wake ukauawa, bali roho yake ikahuishwa". Hii ina maana kwamba dhambi iliyoishi katika asili yake ya kibinadamu (ambayo pia inaitwa mwili) alipokuwa hapa duniani “iliuawa,” na matokeo yake ni kwamba roho yake ilihuishwa. Yesu Kristo sasa anafanya kazi hii hiyo ndani yetu na kwa njia hii tunaumbwa kuwa mahali ambapo Mungu anaweza kuishi kwa njia ya Roho wake.

Soma pia: “Je, Kristo amekuja katika mwili?”

Mungu anataka kumiliki roho aliyotupa. Na Mungu anapokuja kuishi katika roho zetu, hatutunzwa na kulindwa tu, bali roho zetu zinafanywa kuwa hai. Kwa nini Mungu anafanya kazi kwa bidii ili kuzifanya roho zetu kuwa hai? Kwa nini tunapaswa kuwa mahali ambapo Mungu anaweza kuishi? Ni nini sababu ya Mungu kwa hili? Ni kwa sababu Mungu ni upendo, na anataka kutubadilisha na tushiriki asili yake.

Wokovu mkuu na mtukufu

Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena. Nami nikauona mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe. Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, na yeye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.’” Ufunuo 21:1-3

Watu hao ambao Mungu ana makao yake ndani yao, wataishi kati ya watu katika nchi mpya. Watu hao ni wa jiji hilo, Yerusalemu Mpya, inayoshuka kutoka mbinguni.

"Na mataifa watatembea katika nuru yake." Ufunuo 21:24. Haya ni mataifa yaliyookoka ambayo hayakujitayarisha kwa namna ambayo yalifanyika kuwa makao ya Mungu, bali yameliitia jina la Bwana ili kupata msaada, na matokeo yake yameokolewa badala ya kupotea milele. Hawajui maana ya kutembea katika mapenzi na Neno la Mungu (hivyo ndivyo unavyoweza kubadilishwa kuwa makao ya Mungu), lakini watu hao ambao ni nyumba za Mungu wanajua hili vizuri sana. Wamejifunza kuenenda katika nuru kama Yeye alivyo katika nuru. Kwa njia hiyo damu ya Kristo ingewasafisha na dhambi zote na kuwafanya kuwa makao ya Mungu. ( 1 Yohana 1:7 )

"Yeye ashindaye atayarithi haya." Ufunuo 21:7.

Wokovu huu ambao tunajifunza kutembea katika mapenzi na Neno la Mungu ni mkuu sana na wa utukufu, kwa hiyo tujitahidi sana kuupata kadiri tuwezavyo tukiwa bado tunatembea kama wasafiri na wageni hapa duniani.

Chapisho hili linapatikana katika

Makala haya yanatokana na makala ya Johan Oscar Smith ambayo yalionekana kwa mara ya kwanza chini ya kichwa cha habari “Mahali pa kukaa pa Mungu” katika jarida la BCC la "Skjulte Skatter" (Hazina Zilizofichwa) mnamo Februari 1941. Imetafsiriwa kutoka kwa Kinorwe na ilichukuliwa kwa ruhusa ya matumizi kwenye tovuti hii. © Hakimiliki ya Stiftelsen Skjulte Skatters Forlag.