Mungu aliniumba jinsi nilivyo!

Mungu aliniumba jinsi nilivyo!

Nilipata furaha kujua kwamba Mungu aliniumba jinsi nilivyo.

31/3/20154 dk

Na Ukristo wa Utendaji

Mungu aliniumba jinsi nilivyo!

7 dak

Anna ni msichana mwenye furaha sana, huru, na mwenye kicheko. Lakini haikuwa hivyo nyakati zote. Alikuwa akihangaika sana kuhusu watu walivyomfikiria. Hili kwa kweli lilimfanya kuwa mtu asiye na furaha. Anasimulia hadithi yake na jinsi haya yote yalivyobadilika.

"Nilikuwa nikifikiria 'Wanafikiria nini kunihusu? Labda hawanipendi,’ n.k. Ningeogopa maoni ya watu nilipofanya mambo. Nilitaka wanipende. Hata katika mambo rahisi, kama chapisho la Instagram, kwa mfano.

Yesu akawa rafiki yangu

“Siku moja nikiwa kanisani, nilisikia ujumbe ambao ulinifanya nisikilize kwa makini.

"Msemaji alisema kwamba Mungu anataka tuwe na maisha yenye furaha. Alisoma kutoka katika Warumi 8:28, ‘Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi Pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake.’

“Nilikuwa nimesikia mstari huu mara nyingi, lakini sasa kwa mara ya kwanza niliona jinsi ulivyohusika katika maisha yangu mwenyewe. Nilikuwa nikiangalia mambo yote vibaya; furaha yangu haikutegemea watu wengine hata kidogo. Ikiwa nilimpenda Mungu, basi hakuna kitu cha kuogopa kutokana na maoni ya wengine kunihusu. Mungu daima alinitakia mema, na mambo yote yangefanya kazi pamoja kwa wema!

“Nilifanya uamuzi kwamba ningeanza kuishi maisha yangu kwa ajili ya Mungu pekee. Nilianza kusoma Biblia na fasihi za Kikristo kadiri nilivyoweza.

“Yesu akawa rafiki yangu, na ningeweza kumwamini Yeye, kumtegemea Yeye. Kile ambacho watu wengine wananifikiria hakina maana tena katika maisha yangu. Kuna muda mwingi unaopotea katika mawazo kama hayo; kwa kweli inaweza kuwa ya ubinafsi sana.”

"Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye Bwana atakuwa salama." Mithali 29:25.

Mtu binafsi katika Mungu

“Nilianza kuona kwamba ni muhimu sana uwe na utu wako, na uishi maisha yako kwa ajili ya Mungu. Watu wako tofauti - wanavaa tofauti, wanatenda tofauti. Mungu anataka niwe mtu binafsi ndani Yake. Mungu ana mpango kwa ajili yetu sote. Nilipoona hivyo, nilielewa kwamba aliniumba kulingana na mpango wake kwangu na maisha yangu, na kwamba anaweza kunitumia jinsi nilivyo!

“Kwa mfano, mimi si mzuri sana katika michezo, na ni rahisi kufikiri kwamba ni lazima nifanye vizuri, kwa sababu watu wengine wengi wa rika langu wako vizuri. Lakini napenda muziki na media. Mungu amenipa hilo, na aliniumba hivyo, kwa nini niwe na wasiwasi kuhusu kutokuwa mzuri katika michezo? Cha muhimu ni kutafuta nafasi yako na kutumia kile ambacho Mungu amekupa kuwa baraka.

“Kwa hiyo niliamua kwamba nilitaka kuwa aina ya mtu ambaye huwa katika hali nzuri kila wakati. Si kwa nje tu, bali kuwa na furaha ya kweli na ya kudumu ndani kabisa ya moyo wangu. Nilijua kwamba hilo liliwezekana tu nilipoishi maisha yangu kwa ajili ya Mungu, na nikaona kwamba katika kuishi kwa ajili ya Mungu, ninaweza pia kuwa baraka na kufanya mema kwa ajili ya wengine.

Hakuna kinachoweza kuiba furaha yangu!

“Inashangaza tu jinsi Mungu anavyofanya kazi; Tayari amefanya muujiza ndani yangu. Nimebadilika sana kutoka nilivyokuwa hapo awali. Sasa ninaweza kuwa na furaha wakati wote. Hakuna kinachoweza kuiba furaha yangu!

“Bado ninashawishika kuwa na wasiwasi kuhusu maoni ya wengine; kujaribiwa kutaka kibali kutoka kwa watu badala ya kutoka kwa Mungu. Lakini sasa ninapigana dhidi ya majaribu haya na siruhusu yawe na nguvu juu yangu au kutawala maisha yangu.

"Kutokubali - hilo ndilo lengo langu. Mara nyingi mimi hufikiria mstari katika Isaya 40:31: ‘Bali wamngojeao Bwana watapata nguvu mpya.’ Tunaweza kuwa na uhusiano pamoja na Mungu siku zote kupitia sala zetu, na tunaweza kupata nguvu siku zote kutoka Kwake. Ninapojaribiwa kuwa na wasiwasi kuhusu kile ambacho watu wanafikiri, jambo la kwanza ninalofanya ni kuomba, kisha ninapata uwezo wa kukabiliana na hali hiyo. Unapaswa kuomba na kuamini.

"Ni furaha ya kweli! Sidanganyi, nimefurahi sana! Hivi sasa mimi ndiye mwenye furaha zaidi ambayo nimewahi kuwa nayo katika maisha yangu!

“Wakati fulani nilisikia mtu fulani akisema, ‘Labda wewe peke yako ndiye Biblia ambayo watu wanaokuzunguka wanasoma.’ Lengo langu ni kuwa hii ‘Biblia inayotembea, inayozungumza’. Kwamba kupitia maisha yangu, kila mtu anayenizunguka anaweza kuona maana ya kuwa na maisha na Yesu.”

Chapisho hili linapatikana katika

Makala haya yanatokana na makala ya Ann Steiner yaliyochapishwa awali kwenye https://activechristianity.org/ na yamebadilishwa kwa ruhusa ya matumizi kwenye tovuti hii.